Social Icons

Sunday 13 October 2013

AFRIKA SASA YAWAKINGIA KIFUA KENYATTA, RUTO NA AL BASHIR.


Addis Ababa. Muungano wa Afrika (AU) umeitaka Mahakama ya Kimataifa ya Uhalifu (ICC) kusitisha kesi dhidi ya wakuu wa nchi walioko madarakani kwa sasa hadi watakapomaliza vipindi vya uongozi wao.

Viongozi walioko madarakani kwa sasa ambao wanakabiliwa na kesi kwenye mahakama hiyo ni Rais Uhuru Kenyatta wa Kenya na makamu wake, William Ruto wanaotuhumiwa kwa makosa ya uchochezi, mauaji na uhalifu dhidi ya ubinadamu baada ya uchaguzi mkuu wa mwaka 2007.

Mwingine ni Rais wa Sudan, Omar al-Bashir ambaye mahakama hiyo imetoa hati ya kukamatwa kwake akihusishwa na matumizi mabaya ya madaraka kwa kuamrisha mauaji ya watu kwenye eneo la Darfur nchini kwake.

Msimamo huo umefikiwa baada ya kikao cha wakuu wa nchi mjini Addis Ababa jana, kilichozima shinikizo la kutaka nchi wanachama wa umoja huo zilizo wanachama wa mkataba wa Roma ulioianzisha mahakama ya ICC mwaka 2002 zijitoe.

Msimamo huo uliosababisha kuitishwa kwa kikao maalumu cha dharura cha AU ilichofanyika juzi na jana ulipingwa vikali na viongozi mbalimbali duniani, akiwemo Jaji Mtanzania aliyeapishwa wiki hii kuwa Jaji wa ICC, Jaji Stephen Bwana ambaye alisema ICC ni wembe kwa viongozi wanaojifanya miungu watu.

“Afrika ina viongozi wengi wazuri, lakini pia tusifiche ukweli kwamba tunao viongozi wa ovyo, ambao wanadhani ni (semi gods) nusu miungu. Wangependa kila kitu kiwe chao tu. Sasa tukisema kwamba nchi zote za Afrika zijiondoe ICC, tunataka kusema kwamba hatufanyi makosa.”

Jaji Bwana ambaye aliapishwa rasmi wiki hii kuwa Jaji wa ICC nchini Cambodia aliongeza kwamba, viongozi hao ‘miungu watu’ wamezifanya taasisi za utoaji haki kwenye nchi zao kuwa dhaifu na kwamba kwa hali hiyo hawawezi kushtakiwa katika mahakama za nchi zao kwa makosa wanayoyafanya.

Viongozi wengine maarufu duniani waliopinga hatua hiyo ni aliyekuwa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa (AU) Kofi Annan ambaye alisema Afrika itaingia kwenye ‘dimbwi la aibu’ na Askofu Desmond Tutu wa Afrika Kusini ambaye alisema viongozi wanaotaka nchi zao zijitoe wanataka kujihalalishia “uuaji uliotukuka”.

Akizungumzia uamuzi wa mkutano huo wa wakuu wan chi jana, Waziri wa Mambo ya Nje wa Ethiopia, Tedros Adhanom Ghebreyesus alisema uamuzi uliofikiwa ni wa kuitaka mahakama hiyo kutowakamata na kuwashtaki viongozi walipo madarakani.

Alisema wakuu wa AU wamekubaliana kuiandikia ICC na kuitaka kusitisha kesi dhidi ya Rais Kenyatta, makamu wake William Ruto na hati ya kukamatwa kwa Rais Bashir kwa sasa.

Tedros ambaye ndiye mwenyekiti wa Baraza Kuu la AU kwa sasa, alisema ICC imeonesha wazi kwamba imejigeuza kuwa chombo cha kisiasa kinacholenga kuiyumbisha Afrika na Waafrika, suala ambalo haliwezi kukubalika. Alisema kutokana na hali hiyo, ICC imeshindwa kutilia maanani maombi ya awali ya AU, hivyo suala hilo kwa sasa litapelekwa kwenye hatua nyingine.

Chanzo Mwananchi.

No comments:

 
 
Blogger Templates