Social Icons

Sunday 17 November 2013

UNAFIKI WA WABUNGE HAWA AIBU KWA TAIFA


KATIKA kipindi cha miaka mitatu iliyopita kumekuwa na kelele nyingi kutoka kwa wabunge, wanaharakati, vyombo vya habari na wananchi wa kulaani mauaji ya tembo. Mbali na kuulani huko, wamekuwa wakiilaumu serikali kwa kutokuchukua hatua muafaka kumaliza tatizo hili.

Wengine wamedai hali ni mbaya, wakitaka sheria itungwe ili majangili wapigwe risasi, wapo waliotaka waziri mwenye dhamana ajiuzulu huku wengine wakilalamika na kutaka tumwachie Mungu!

Ni kweli hali ya ujangili dhidi ya tembo nchini imekithiri na hakuna mbadala zaidi ya kuchukua hatua muafaka. Waziri mwenye dhamana, Balozi Khamisi Kagasheki, akiweka wazi hili katika Bunge la bajeti lililopita alihadharisha kuwa inaandaliwa operesheni maalumu.

Kwamba ‘Operesheni Uhai’ iliyofanyika mwishoni mwa miaka ya 1980 ingekuwa ndogo kulinganisha na hiyo iliyokuwa ikiandaliwa.

Katika utatuzi wa tatizo lolote kuna mbinu kuu tatu. Mbinu za kawaida ambazo ni endelevu (proactive), mbinu zinazolenga kuzuia tatizo (preventive au deterrent) na mbinu za kujibu mapigo (reactive).

Wakati mbinu mbili za kwanza zinatoa muda mrefu wa kujipanga na aghalabu huwa shirikishi, mbinu ya tatu ni ya haraka na inachukua sura ya udharura na pengine haitoi fursa kwa demokrasia.

Kwa mfano, kinapozuka kipindupindu mahali au nyumba inapoungua huwezi kuahirisha hatua ili kungoja ridhaa ya kikao au kuandaa semina kuelimisha watu namna ya kukabili tatizo.

Ni kweli kwamba mbinu mbili zilizotajwa hapo juu (proactive na preventive) zimekuwa zinatumiwa na mamlaka husika kupambana na tatizo la mauaji ya tembo. Hata hivyo, sababu kadhaa zimegeuza ujangili wa tembo kuwa janga na hivyo kufanya njia hizi mbili zisiwe ‘toshelevu’.

Tembo wengi wanauawa kutokana na kukua kwa soko katika nchi za mashariki ya mbali. Aidha, ongezeko la wageni kutoka katika nchi hizi; ongezeko la wahamiaji haramu na urahisi wa wahalifu kupata silaha za kivita; kushuka kwa maadili na uzalendo miongoni mwa Watanzania watumishi na wasio watumishi; kuimarika kwa miundombinu (barabara) na njia za mawasiliano (simu za mikononi) na jiografia yetu (kupakana na Bahari ya Hindi) ni mambo yanayochangia ongezeko la mauaji ya tembo na biashara haramu ya meno yake.

Katika hali ambayo tembo wengi wanakufa kila siku kiasi cha kutishia uwepo wake katika miaka michache ijayo, hakuna njia nyingine yoyote ya kukabili tatizo hili zaidi ya kuchukua hatua za dharura na haraka (reactive measures). Na hili ndilo lililofanywa na serikali kupitia kwa waziri mwenye dhamana ambaye alitangaza ‘Operesheni Tokomeza’.

Naamini hatua hii ni ya kupongezwa. Waziri Kagasheki amethubutu na nina hakika akisaidiwa na kuungwa mkono ataweza. Kuna wanaodai operesheni hii si suluhisho. Kwa bahati mbaya Watanzania tumekuwa wepesi kukosoa bila kutoa suluhisho mbadala. Ni vema wale wanaokosoa wakatuambia dawa mujarabu ya kumaliza tatizo hili ni ipi.

Wakati matunda ya operesheni hii yameanza kuonekana, inashangaza wanapojitokeza wanasiasa na ‘wanaojiita wanaharakati’ kumshambulia waziri ambaye wengi wanaomfahamu hawajawahi kutilia shaka uadilifu na utendaji wake kwa umma.

Kimsingi, wanasiasa na wanaharakati hawajamtendea haki Kagasheki, hawajazitendea haki maliasili zetu na hawajaitendea haki nchi hii. Ninachokiona hapa ni baadhi ya wanasiasa kutumia mbinu chafu kujijenga kisiasa. Lakini pia kuna uwezekano kuwa wapinzani wa vita hii wana maslahi kutokana na wao binafsi au jamaa zao kuhusika katika dhambi hii kubwa ya kuangamiza tembo.

Ama nyingi ya asasi (NGOs) zinazodai kutetea haki za binadamu inaeleweka kuwa nyingi zipo, si kwa maslahi hasa ya Watanzania, lakini ni mashine za watu za kuvuna pesa. Asasi hizi, mara nyingi zimekuwa zikiunda hoja hasi dhidi ya serikali ili kujenga uhalali wa kupata pesa kutoka kwa wafadhili wao na ndio maana watendaji wake wana utajiri wa kutisha.

Wangekuwa wakweli wangeonesha pia kusikitishwa na vifo vya askari waliokufa kwa kuuawa na majangili. Inakuwaje mtu kulalamikia ng’ombe kukamatwa ndani ya hifadhi lakini asiguswe na vifo vya binadamu vinavyosababishwa na majangili? Huo uzalendo uko wapi? Ni vema asasi hizi zikaendelea kuwepo na kutengeneza pesa, lakini si kwa mbinu chafu kama hizo.

Kauli ya mbunge mmoja kuwa eti “..watu waliokamatwa ndani ya hifadhi wamepigwa na kuumizwa wakati majangili wa tembo wameachwa” si kwamba tu inakatisha tamaa, bali pia inaonesha ni aina gani ya wabunge tulinao.

Mbunge angewasaidia Watanzania kama angetuambia waliokamatwa ndani ya hifadhi walifuata nini na kwa sheria gani. Aidha, alitakiwa kutusaidia kuwa majangili wa tembo wanaohusika ni kina nani hasa! Ieleweke kuwa hii vita si ya Kagasheki peke yake.

Hivyo hao wanaowajua majangili wamsaidie ili sheria ichukue mkondo wake. Sasa mbunge aliyekula kiapo cha kuilinda katiba na kutumikia umma anapojua wahujumu kama hao halafu akakaa kimya mpaka Kagasheki aje awajue, anatoa matumaini gani kwa Watanzania?

Kwa tafsiri yangu, mbunge wa namna hii ni msaliti wa nchi yetu. Mwingine, tena waziri analalamikia msaidizi wake kukamatwa. Hivi msaidizi wako akituhumiwa kwa uhalifu ana kinga gani ya kutokukamatwa na kuhojiwa?

Operesheni yoyote ile duniani kote inapotokea huwa kuna kasoro za hapa na pale. Hata nchi zilizoendelea zimejikuta zikifanya makosa katika operesheni kama hizi na pengine hata kusababisha watu wake kupoteza maisha (rejea Marekani na vita ya magaidi).

Lakini pia hata kwenye sayansi za tiba karibu dawa zote huwa na madhara ya kando (side effects) lakini baadaye hupatikana tiba ya kudumu. Labda wanasiasa na wanaharakati wetu wangetusaidia sana kama wangetupa mfano wa operesheni yoyote ile ambayo haikuwahi kuwa na kasoro.

Hata hivyo, kama wote tunakubali kuwa mapambano dhidi ya ujangili wa tembo ni vita ya lazima, hivi kukijitokeza kasoro unaamua kuachana na hiyo vita? Inapotokea unasafiri kwa gari ikapata pancha, unaamua kuachana na safari na kumfukuza dereva?

Binafsi sitaki kuamini wale wanaomshambulia Waziri Kagasheki wana uchungu na nia ya dhati na maisha ya Watanzania wenzao. Ninachoamini ni kwamba kuna ajenda iliyojificha. Nashawishika kuamini hivyo kwa kuwa ni wabunge hawa hawa waliokuwa wanapiga kelele kwamba tembo wanakwisha, sasa wamemgeuka Balozi Kagasheki.

Leo Balozi Kagasheki anapofanya kweli wabunge hao hao wanadai ajiuzulu kwa kuvunja haki za binadamu! Hivi huu unafiki wa wabunge wetu utaisha lini? Hivi maslahi gani ya nchi wanayopigania?

Pale Kagasheki alipotangaza kusitisha ‘Operesheni Tokomeza’ (tangazo ambalo nahisi pengine hata yeye hakulifanya kwa ridhaa yake), sikutarajia wabunge wangekubaliana nalo. Cha ajabu, wengi waliochangia tamko hili la wizara walijielekeza kwenye lawama dhidi yake na wahusika wengine kwenye operesheni hii na kuonyesha kuguswa kwa masikitiko na kitendo cha ng’ombe pamoja na watu kukamatwa.

Katika michango yote, wabunge wengi wakiwemo wale wanaopenda kujipambanua kama wazalendo hawakuonyesha kukerwa na mauaji ya tembo! Hili linazua maswali. Je, kelele zote walizokuwa wakipiga dhidi ya ujangili zililenga kukejeli wananchi kwamba wana uchungu na rasilimali za taifa?

Je, katika hali kama hii ambapo wanaonyesha wazi kupinga operesheni, ni kitu gani kitasababisha tusiwaunganishe na mtandao wa ujangili? Je, kwa nini tusiamini kuwa lawama zote na chuki zinazoelekezwa kwa Balozi Kagasheki zimejificha kwenye maslahi ya kisiasa zaidi?

Nawasihi Watanzania wote wenye nia njema na hatima ya maliasili zetu kuendelea kuunga mkono kwa nguvu zote juhudi za kupambana dhidi ya janga la ujangili wa tembo na rasilimali nyingine za taifa. Tuwe makini na wanasiasa wanafiki wanaotumia shida, misiba na majanga yetu kujinufaisha kisiasa.

Namsihi Waziri Kagasheki na watendaji wengine wote wenye mtazamo chanya kwa taifa letu wasikatishwe tamaa. Ieleweke kuwa, katika hali ambayo watu wameingia kwenye siasa kwa mbinu chafu, si rahisi kwa watu waadilifu, makini na wenye viwango vya hali ya juu vya utendaji kama Balozi Kagasheki kukubalika.

Watapigwa vita na kuchafuliwa bila sababu za msingi. Imani kubwa iko kwa Rais Jakaya Kikwete, ambaye ndiye aliyempa dhamana Waziri Kagasheki.

Hotuba yake aliyotoa bungeni, inatoa matumaini kwamba fitna na chuki zinazoelekezwa kwa Balozi Kagasheki na wasioitakia mema nchi yetu kwa kivuli cha uzalendo na kutetea haki za binadamu zitashindwa.

                                                      Mungu Ibariki Tanzania.


Chanzo:- RaiaMwema

1 comment:

Mpaju said...

Makala safi sana. Hakuna cha kuongeza kwangu.

 
 
Blogger Templates