Social Icons

Monday 8 September 2014

HADITHI: Missed call ya shemeji -5


“Majangaa…majangaa…mbona majangaa,” aliendelea kuimba dada mtu kwenye eneo la kibwagizo cha wimbo huo, kisha wote wakacheka sana, ghafla dada mtu akasema...
SASA ENDELEA….

“Nikwambie kitu mdogo wangu?”
“Niambie.”
“Unajua umepata bahati sana kuolewa, mshukuru Mungu kwa sababu heshima ya mwanamke ni kuolewa na si kufanya kazi. Hata kule nyumbani kijijini we unajua, msichana kukaa kwao mpaka umri unapita ni aibu, ndiyo maana wengi hujikuta wakiingia hata kwenye ndoa isiyo sahihi ilimradi aonekane ameolewa.”

“Unaposema ndoa siyo sahihi unamaanisha nini dada?”
“Namaanisha msichana anatoka nyumbani kwenda kuishi kwa mwanaume bila ndoa wala mahari. Au msichana anaamua kuzaa ili mwanaume amchukue wakaishi wote.”
Aisha alihema kwa nguvu kwanza kisha akamwangalia dada yake huyo na kusema…
“Mimi binafsi sijapenda kuolewa.”

“He! Unatania au uko siriasi mdogo wangu?”
“Niko siriasi.”
“Kwa nini?”

“Sipendi mambo ya kuombana unyumba usiku wakati watu tunataka kulala.”
“Unamaanisha nini?”
“Namaanisha kwamba, kuwa huru ni vizuri sana kuliko kuwa na mume.”
“Kwa hiyo unaombea ndoa yako ife hata leo?”

“Siwezi kusema hivyo kwani kama ulivyosema ndoa ni heshima katika jamii. Mwanamke hata ukiwa na fedha vipi, kama huna mume huna heshima. Tofauti na mwanaume, anaweza kuwa tajiri akawa hana mke lakini jamii inampa heshima yake kama kawaida.”
“Mh! Leo umeniambia jambo zito sana mdogo wangu, kwamba hupendi mambo ya kuombana unyumba? Sasa mwenzio aende wapi?”
“Asiende kokote, avumilie hadi mimi nipende.”
“Hata kama mwezi?”

“Hata miezi miwili mpaka mitatu.”
“Sijapata kuona.”

***
Wakati wa kula, dada ake Aisha akaanza…
“Mke wangu leo chakula kizuri sana, daa!”
“Umeona kazi yangu mume wangu, ni kitamu eee?”
“Kwa kweli ni kitamu sana mke wangu, natamani usiondoke hapa nyumbani.”
“Mbona nimefika mume wangu. Wewe tu unitunze.”
“Nitakutunza hadi kifo.”
“Eee, safi sana.”

“Sasa nisipokutunza wewe nani mwingine mke wangu?”
“Hakuna, mimi ndiyo mama watoto wako. Na mimi nakuahidi kukutii.”
“Umeonaee?”

“Basi mpeane vyote, maana vingine Beka hapati kwa wakati anaotaka yeye,” Aisha alidakia kwa sauti iliyojaa mikato. Kwa mbali mazungumzo hayo hakuyapenda, baadhi ya vipengele kama…
“Kwa kweli ni kitamu sana mke wangu, natamani usiondoke hapa nyumbani.”
Aisha aliumia kwa sababu ni kweli chakula kile alikipika dada yake huyo kwa hiyo alihisi wivu kwa sababu nadra sana mume wake kumsifia yeye na kwa vile mumewe hakujua nani amekipika ina maana aliona tofauti ya siku zote na siku hiyo.

“He! Yamekuwa hayo mdogo wangu?” dada mtu alishangaa, moyoni alicheka kusikia mdogo wake amekiongea kitu cha kweli kwa vile alishatoka kumwambia muda mfupi nyuma.
“Mimi sijawahi kusifiwa, leo wewe umesifiwa.”
“Jamani! Kwani kosa liko wapi?”
“Hakuna kosa dada, wala mimi sikulaumu wewe, namshangaa shemejio kutowahi kusifia chakula cha kukipika mimi hata siku moja.”
“Sasa nitakisifia wakati hakina sababu ya kupewa hiyo sifa?” alidakia Beka huku akiachia tabasamu lililojaa kejeli kwa mbali.

“Una maana siwezi kupika?”
“Siyo kwamba huwezi, bali hujui. Kuweza unaweza.”
Aisha alipandisha hasira, alitamani asimame na kumnyanyua mume wake hadi chumbani ili akamweleze vizuri…

“Una maana gani?” aliuliza Aisha.
“Nina maana kwamba,  hujui nini kikianza chakula kitakuwa na ladha fulani, si ajabu unaanza kukaanga chumvi badala ya vitunguu kisha nyanya.”
Aisha alinawa maji kabla hajashiba kisha akatoka kwenye meza ya chakula.
“Aisha,” aliita dada mtu.

“Nimeshiba, nyie kuleni tu, si mke na mume bwana,” alijibu Aisha huku akienda kukaa kwenye sofa na kuangalia tivii. Chaneli hazikuwa zinapanda kichwani lakini ilimradi tu.
Dada mtu na shemeji yake waliangaliana kwa macho yenye maswali na kicheko lakini hakuna aliyetoa sauti kwa mwenzake. Mwisho dada mtu huyo akamminyia jicho moja shemejiye, naye akaangalia chini ili kujizuia asicheke.

Beka naye aliamua kunawa, akatoka kwenda chumbani ambako aliamua kupanda kitandani ili kuusaka usingizi lakini kabla haujampata, meseji iliingia kwenye simu yake ikitoka kwa shemeji mtu…
“Unalo hilo shemeji, amenunaje hapa!”
Beka alicheka, akajibu…

“Sina hofu sana maana najua wewe upo.”
“Mh! Na mimi nakwenda kujilalia zangu.”
“Kalale, lakini kabla hujalala nitumie meseji moja nzurinzuri ili na mimi nilale vizuri kama wewe.”
“Poa shem.”

Baada ya nusu saa, kweli meseji iliingia kwenye simu ya Beka kutoka kwa shemeji yake…
“Mimi nalala mume wangu, lala salama na wewe, nakupenda sana mkeo.”
“Nakupenda pia mumeo, natamani ningelala na wewe.”
“Ha! Ha! Huna ubavu huo utabaki kutamani kama ulivyosema.”
“Naweza kujilipua.”
“Kivipi?”

“Kuna kichwakichwa.”
“Ukimaanisha?”
“Nikimaanisha ajue asijue.”
“Wewee. Huwezi.”

“Unabisha nije?”
“Sibishi bwana, usije ukaja kweli ikawa noma.”
“Mi hamnazo unajua.”
“Teh! Teh!”

Inaendelea.

Chanzo globalpublishers


No comments:

 
 
Blogger Templates