Social Icons

Friday, 20 September 2013

WAZIRI CHIKAWE ATOBOA SIRI YA BUNGE.


WAKATI fukuto la mjadala wa Muswada wa Sheria ya Mabadiliko ya Katiba Mpya linaendelea, Waziri wa Katiba na Sheria, Mathias Chikawe ameiumbua Kamati ya Bunge ya Katiba, Sheria na Utawala. Akizungumza mjini Dar es Salaam jana, wakati akikagua mradi wa ujenzi wa jengo la ghorofa 26 la Wakala wa Usajili, Ufilisi na Udhamini (RITA), Waziri Chikawe alisema kamati hiyo inayoongozwa na Mwenyekiti wake, Pindi Chana haikufika Zanzibar kupata maoni ya wadau.

Kauli hiyo, inakinzana na taarifa aliyoitoa Chana bungeni hivi karibuni, kuwa kamati yake ilikwenda Zanzibar na kualika wajumbe mbalimbali, wakiwamo Wazanzibari, Mkurugenzi wa Tume ya Uchaguzi Zanzibar (ZEC), Chama cha Wanasheria wa Zanzibar pamoja na maofisa wa ZEC, ambao alisema wote walitoa maoni yao mbele ya kamati hiyo.

Alisema, licha ya kamati hiyo kutofika Zanzibar, hakuna sheria inayoitaka kupeleka muswada wowote kwa wananchi, kama inavyodaiwa.

“Ni utaratibu tu uliopangwa na kamati, hakuna sheria inayoitaka Kamati kupeleka muswada kwa wananchi. 

“Siwezi kuzungumzia kazi za kamati kwa sababu ni mhimili unaojitegemea, bali nazungumzia kwa mujibu wa sheria,” alisema Chikawe.

“Mei 25, mwaka huu Serikali ilipokea maoni kutoka Zanzibar na kuyafanyia kazi.

“Kimsingi si sheria muswada wowote unaopitishwa uende kwa wananchi, sheria zinatungwa na Bunge huo ndio utaratibu,” alisema Chikawe.

Alisema pamoja na mizengwe iliyotokea bungeni hivi karibuni ambayo ilisababisha wabunge wa upinzani kuungana na kususia mjadala wa muswada huo, mchakato huo uliendelea vizuri kilichobaki ni Rais Jakaya Kikwete kusaini muswada huo.

Alisema atamshangaa rais kama hatasaini muswada huo na kwamba atakuwa ametafuta mgogoro na wabunge kwa kuingilia shughuli za Bunge.

Mbali na hivyo, alisema vitisho vinavyotolewa na wapinzani kumtisha rais kuwa akisaini muswada huo yatatokea machafuko, havina mashiko.

“Kuna watu wanasema rais akisaini muswada fujo zitatokea, fujo sio mvua waseme wazi kuwa sisi tutafanya fujo, nitashangaa sana kama rais hatasaini.

“Hakuna makosa yoyote yaliyofanyika, utaratibu umefuatwa kama kuna kitu hakipo sawa waeleze nini kifanyike walete mawazo yao badala ya kupeleka malalamiko jangwani, kutasaidia nini wakati sheria imeshapita? Alihoji Chikawe.

Wahamiaji haramu 

Wakati huo huo Waziri Chikawe, ameisafisha RITA, na kudai kuwa taarifa zinazotolewa kuwa wakala hiyo inatoa vyeti vya kuzaliwa kwa wahamiaji haramu si za kweli.

Hatua hiyo imetokana na madai yaliyotolewa hivi karibuni na Ofisa wa Idara ya Uhamiaji Mkoa wa Dar es Salaam, Grace Hokororo kuwa wakala hiyo imetoa vyeti kwa wahamiaji haramu. 

“Kuna maneno tunayasikia wakati huu wa mchakato wa kuwaondoa wahamiaji haramu, kuwa RITA inatoa uraia.

“Naomba ieleweke kuwa RITA haitoi uraia, bali inaandikisha vizazi na vifo vyote na kutoa vyeti vya ndoa, suala la uraia lina mamlaka yake ambayo ni Idara ya Uhamiaji iliyo chini ya Wizara ya Mambo ya Ndani Nchi,” alisema Chikawe.

Alisema jukumu la RITA ni kutoa vyeti vya kuzaliwa kwa yeyote anayezaliwa katika ardhi ya Tanzania, hata kama amezaliwa na raia wa taifa jingine.

“Mfano mwingine upo katika vitambulisho vya taifa, NIDA inaweza kutoa kitambulisho kwa mtu yeyote,” alisema Waziri huyo.

Jengo hilo la RITA linatarajia kugharimu zaidi ya Sh bilioni 35.86, fedha ambazo zimetolewa na Shirika la Taifa la Hifadhi ya Jamii (NSSF), linatarajiwa kuzinduliwa na Rais Jakaya Kikwete mwishoni mwa mwaka huu.

Chanzo:- Mtanzania.

No comments:

 
 
Blogger Templates