Social Icons

Tuesday, 20 June 2017

SIMULIZI: Nilipanga nyumba moja na majini - 2



Na Irene Mwamfupe Ndauka. 
 ILIPOISHIA WIKI ILIYOPITA:Nilichukua kama saa moja kutoka kazini hadi kufika nyumbani. Nje nilikuta mfuko wa rambo  mweusi, ndani yake ulionekana kuwa na kitu kwani ulikuwa umetuna sana. Niliinama kuipekenyua ili nijue ndani kulikuwa na nini, nilishangaa kuona ni vipande vya nyama za kuchoma tena vilikuwa na moto.

“Kha! Atakuwa nani ameweka?” nilijiuliza mwenyewe, nikauacha palepale, mimi nikapanda ngazi za kuingia ndani. Mlango ulikuwa wazi hali iliyoashiria kwamba, wenzangu walisharudi. Nilisukuma mlango, nikaingia. Nilikutana na harufu ya pafyumu, nikahisi walikuwa wakijiandaa kutoka.
 ("Kitabu cha Niliyoyaona Mochwari Sitasahau kinapatikana sehemu zote za Tanzania kwa wauza Magazeti ni Tsh 3000/=tu")

“Jamani za leo?” nilisalimia kwa sauti ya juu licha ya kwamba, mlango wao ulikuwa umefungwa, hakuna aliyeniitikia, hilo sikulijali sana kwani niliamini kwa kuwa walikuwa ndani, isingekuwa rahisi wasikie salamu yangu.

Niliingia sebuleni kwangu, kisha nikaenda chumbani, kuna kitu kilinishangaza, nikasimama kwa mshtuko. Nilikuta sehemu nilipoweka kiberiti asubuhi siyo, nilikiacha juu ya meza, nikakikuta juu ya kitanda. Niliacha kioo na kitana juu ya kitanda, lakini nikavikuta kwenye stuli, niliguna!

Nilikishika kioo cha kukiangalia kwa umakini kama kina mabadiliko yoyote, lakini sikuona, nikashika kitana. Nilipokigaua sana pia sikuona kitu cha tofauti, nikaamua kuchania, nikahisi kuguswa na kitu kama nywele ndefu kama za mtu aliyefuga. Nilikiweka kitana juu usawa wa dirishani, nikaona nywelenywele nene, nyeusi, mwili wote ukasisimka.

Ninavyojua mimi, mwanamke mwenye nywele nyingi akichania kitana, ndiyo huacha nywele, sasa mimi nilikuwa na nywele fupi sana zisingeweza kuacha nywele ndefu kwenye kitana.

“Mh! Hapa kuna kinachoendelea,” nilisema moyoni huku nikikaa. Nilishtuka zaidi kuona soksi zikiwa kwenye msumari nyuma ya mlango wakati niliacha chini.

“Huyu ni nani?” niliuliza kwa sauti ya ukali.
Ghafla nikasikia kicheko kutoka chumbani kwa wale wenzangu.
Nilikaa kwenye kochi, nikaanza kuangalia sehemu mbalimbali za mle ndani ambazo niliamini naweza kuona mabadiliko mengine mbali na yale ambayo nilishayaona, lakini sikubahatika.

Nilitoka, nikaenda sebuleni ambako nako nilianza kuangalia kila kona ya sebule. Nilishangaa kuona glasi ya maji ya kunywa ambayo niliitumia asubuhi kisha nikaacha maji yamejaa, ikiwa haina hata tone la maji mbaya zaidi, iliwekwa juu ya kabati ambapo mimi niliiweka kwenye meza ya katikati ya sebule.

“Mh! Hii kali sasa,” nilijikuta nikisema kwa sauti, mara nikasikia kicheko tena kutokea upande wa pili kule kwa wenzangu. Sasa nikaanza kama kuhisi kitu kuhusu watu hao. Ni kwanini kila nilipoongea kwa sauti ndipo na wao waliangua kicheko?
Niliamua kujaribu tena, nikasema kwa sauti:

“Nitakuja kuua mtu, kweli tena.” Nikasikia kicheko tena, safari hii kilidumu kwa muda.
Moyoni nikasema naanza kufanyia kazi uhusiano wa maneno yangu na vicheko vya wale majirani. Nilitoka kurudi chumbani, wakati napita kwenye korido, nilisimama jirani na mlango wao. Walikuwa wakiongea, lakini niliposimama mimi, kukawa kimya ghafla kama hakuna watu.

Nilipozama chumbani, nyuma wakaanza kuongea tena. Sikufunga mlango ili niweze kusikia wanachokiongea, lakini jamani kwa kusema ule ukweli wa Mungu, sikujua walikuwa wakitumia lugha gani katika kuwasiliana hata pale nilipojitahidi kutega masikio kwa umakini wa hali ya juu sana.

Kuna wakati utadhani wanatumia sana neno dotikom, lakini ukisema usikilize zaidi unasikia wakisema sana kotoko au kiburate, wakati mwingine sauti ya kike ilisema kaunto, ya kiume ikarudia hivyohivyo, kaunto.

Nia yangu kubwa ilikuwa kuwaona kwa sura na kufahamu kama ni ngozi nyeusi au nyeupe. Hilo peke yake lingenipa mwanga ni watu wa aina gani naishi nao pale ndani ya nyumba.
Nilisikia mlango wa chumbani kwao ukifunguliwa na mimi nikatoka haraka sana, cha ajabu sikuona mtu akitoka lakini mlangoni kulikuwa na kandambili pea moja tu wakati zilikuwa pea mbili.

Hilo lilimaanisha kwamba, mmoja wao alitoka kwenda chooni, nilichofanya ni kuamua kusimama katikati ya mlango wangu ili huyo aliyekwenda chooni akirudi nimuone. Ni kweli mmoja wao alikwenda chooni kwani nilisikia mlio wa maji.

Nilijiahidi kusimama mlangoni kwangu kumsubiria. Kwa ramani ya nyumba ile ilivyo, asingeweza kutoka chooni bila mimi kumwona hata kama angekuwa anataka kutoka kwenda nje au uani.

Mlio wa maji ulikosa kusikika, nikawa natumbulia macho kule huku moyoni nikisema:
“Leo ndiyo leo, asemaye kesho mwongo, hata afanyaje, hawezi kunichenga hapa hata kidogo,” nilisema moyoni, ingawa wakati huo mapigo ya moyo yalikuwa yakinienda kwa kasi.

Nilipoanza kuhisi muda unakwenda na hakuna mtu aliyetoka, nikampa dakika tatu kwamba lazima atakuwa anavaa ndiyo maana anachelewa:

“Labda alikuwa anajisaidia haja kubwa, maana wengine huwa wanavua nguo zote, lakini mimi nipo, siendi kokote,” nilisema moyoni nikiwa bado nimesimama mlangoni kwangu.
Baaad ya muda, nikasikia watu wakiongea chumbani kwao, nikashtuka, nilijikuta nikisema:
“Haa!”

Haraka sana nilitupa macho mlangoni kuangalia kandambili, nikazikuta pea mbili, nikashangaa:

“Ina maana amenipita hapahapa au? Haiwezekani, asingeweza kunipita hata kama ingekuwaje?” niliwaza. Nilitoka kuelekea chooni, nikakuta mlango uko wazi, nikachungulia ndani, hakukuwa na mtu, nikanyoosha mikoni, nikarudi ndani.
Nilifikia kwenye kochi sebuleni, nikahema kwa nguvu kwani niliamini nimo ndani ya miujiza mikubwa ya ndani ya nyumba ile.

“Hivi ni kwanini dalali alinidanganya hivi?” nilijiuliza mwenyewe nikiamini kwamba, dalali aliyenipangisha nyumba ile alijua mchezo mzima ila alitaka kupata fedha tu ndiyo maana alinipangisha bila kunipa tahadhari.

Nilitoka sebuleni, nikaenda chumbani, kitandani nikakuta ‘toilet paper’ ikiwa imekatwa sehemu. Mimi niliicha pembeni ya dirisha, lakini ikaonesha kuna mtu aliichukua na kunyofoa kidogo kisha badala ya kuirudishia palepale, yeye aliiacha kitandani.

Mbali na ‘toilet paper’ pia kuna kikopo chenye vijiti vyenye pamba za masikio kilikuwa kwenye stuli jirani na kitanda, lakini kwa muda huo kilikuwa kimeanguka chini halafu vijiti vimebaki kama vitatu tu kwa maana kwamba, aliyeingia kuchukua ‘toilet paper’ ndiyo huyohuyo aliyechota vijiti vya pamba.

SIMULIZI: Nilipanga nyumba moja na majini -1



 Na IRENE MWAMFUPE NDAUKA
“KAMA kuna watu hawayajui haya nitakayoyaongea basi nawataka kuanzia sasa wajue kwamba, hapa Dar kuna mambo makubwa sana ambayo ukisimuliwa unaweza kusema si kweli, lakini wale wanaoyapata wanajua. Ila wewe omba yasikukute hata siku moja...”

Ndivyo alivyoanza kusimulia Bw. Humuli Samaki (43), mkazi wa Buguruni (kwa sasa) ambaye alipata mkasa mzito akidai alipanga nyumba moja na majini Magomeni, Dar es Salaam. Anaendelea…

“Si zamani sana mkasa huu uliponitokea, ilikuwa mwaka 2009 tu. Kwa hiyo naweza kusema ni juzijuzi.  Kwa sasa naishi hapa Buguruni, baada ya kuhama kutoka Magomeni ambako nilipataka mkasa huo mzito na wa kuogopesha. Nilipanga nyumba moja na majini.”

Awali nilikuwa nikiishi Mwananyamala Mwinjuma, jirani kabisa na Makao Makuu ya Bendi ya TOT, hata Kapteni John Komba nilizoeana naye kwa kuonanaonana pale CCM-Mwinjuma, ingawa jina langu najua hakuwa akilifahamu.

Nyumba niliyokuwa nikiishi Mwananyamala iliingia kwenye mgogoro wa mirathi, familia ilifika mahakamani. Hukumu ilipotoka ikaamriwa iuzwe kisha ndugu wagawane fedha.

Kwa maana hiyo, mimi na wapangaji wenzangu watano, tulipewa notisi ya kuhama baada ya mteja kupatikana. Huyu mteja anaitwa Masawe anafanya kazi Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) lakini sijui ofisi za wapi.

Ilibidi mimi niangalie mwelekeo mwingine, niliamua nibadili upepo, nikatamani kwenda kuishi Magomeni. Kwa wakati huo nilikuwa sina familia. Sina mke wala mtoto, hata wa kusingiziwa. Kwa hiyo nilikuwa naishi peke yangu. Ni mwaka jana ndiyo nimeoa mke wangu huyu.

Rafiki yangu mmoja anaitwa Mohammed Kombe alinipa namba ya dalali kwani yeye anaishi Magomeni hata sasa. Nilimpigia simu dalali wake, anaitwa Yusuf Mwamba, akaniita Magomeni pale kwenye nyumba wanayosema aliwahi kuishi Baba wa Taifa, hayati Mwalimu Julius Nyerere.

Nilikwenda mpaka pale, nilimkuta amesimama nje ya nyumba hiyo, tukasalimiana, akaniuliza nataka nyumba yenye sifa gani, nikamweleza.

Akasema nyumba ya aina hiyo ipo moja mitaa ya katikati kama unatokea pale tulipo kuelekea kwa Sheikh Yahya Hussein (marehemu).

Tulikwenda kuiona hiyo nyumba. Wakati tukiwa tunaifikia, nilishangaa kuwaona majirani wakitukodolea macho si kawaida, sikushangaa sana nikijua ni mambo ya mjini kitu kidogo tu watu kibao.

Yule dalali alifungua mlango, tukaingia ndani. Tulipita sebuleni, tukaenda kwenye vyumba viwili, tukaelekea  jikoni, chooni na kumalizia bafuni. Ni nyumba iliyojitegemea kwa maana kwamba, ilikuwa na ua wake na mtu akiwa uani hakuna kuona nje. Mlango wa kuingilia ndani ni mmoja tu.

Kulikuwa na vyumba vingine viwili ambavyo toka mwanzo dalali aliniambia chumba kuna mwanaume anaishi na mkewe. Chumba kimoja wanalala, kingine wamekifanya sebuleni, lakini hawana watoto kama mimi.

Nilijiridhisha kwamba ni pazuri, dalali akaniuliza kuhusu malipo, nikamwambia tuongozane nikachukue pesa Magomeni Mapipa kwenye Benki ya Barclays, akasema wakati mimi nakwenda kutoa hizo pesa, yeye anakwenda Dawasco Tawi la Magomeni na shida muhimu pale.

Tukiwa tunaelekea Magomeni Mapipa, nilimuuliza wenye vile vyumba wanafanya kazi wapi? Akajibu wafanyabiashara, lakini hata yeye hajui ni wapi. Nilimuuliza imekuwaje ana funguo, wale wapangaji wengine wakirudi je, akajibu wana funguo yao na ile yeye alipewa na mwenye nyumba kwa ajili ya kutafutia mpangaji mwingine. Nilikubaliana naye.

***
Baada ya nusu saa nilitoka benki nikiwa na hela, nikampigia simu, akasema na yeye alishatoka Dawasco na wakati huo alikuwa anakunywa soda kwenye Hoteli ya Shibam, ipo palepale Mapipa. Nilimfuata pale, nikampa fedha, akatoa mkataba, nikajaza kwani yeye ndiye aliyepewa jukumu lote na mwenye nyumba.
“Kwa hiyo upo huru kwenda kuhamia,” dalali aliniambia huku akinikabidhi funguo.
“Sawa, nitahamia usiku wa leo.”
Nilirudi nyumbani kwa awali na kupangapanga vitu tayari kwa usiku kuhamia makazi mapya, Magomeni. Niliwaambia wapangaji wenzangu wote, nao wakanitakia maisha mema huku wakisema tukumbukane kwani hata wao walikuwa kwenye mchakato wa kuhama kwenye nyumba ile.

***
Saa mbili usiku nilikuwa juu ya lori tukipeleka mizigo makazi mapya, lakini moyoni nilikuwa na maswali mengi ambayo mpaka leo hii siyakumbuki na yalikosa majibu. Pia, nilijikuta nakosa amani ya moyo na sikujua ni kwanini!

Nje, nilikuta taa inawaka, ndani pia taa inawaka, lakini si sebuleni bali kwenye korido. Hii iliashiria kwamba, wale wapangaji wenzangu walisharudi kutoka kwenye biashara zao.

Nilishusha vyombo kwa kusaidiwa na wasaidizi wa dereva wa lile lori, lakini nilishangaa sana kuona kila nikiingia na mizigo, wale wapangaji wenzangu wanacheka sana chumbani kwao. Maana yangu ni kwamba, kwa kawaida walitakiwa hata watoke na kunisalimia ili tufahamiane. Tena kwa wengine, mume angetoka na kunisaidia kubeba hata stuli tu.
Ilifika mahali, wale vijana waliokuwa wakinisaidia waliniuliza:

“Hivi hao majirani zako mbona hawatoki, wanacheka tu chumbani.”
Niliwajibu mimi mwenyewe sijui, lakini sikumaindi sana. Akaja mama mmoja aliyesema anaishi nyumba ya pili, akasalimia na kuniuliza maswali.
“Hamjambo wanangu?”

Tuliitikia wote, akauliza nani anahamia pale kati ya sisi wote, tulikuwa watano mbali na dereva.
“Ni mimi.”
“Ooo, mzima baba?”
“Mimi mzima mama.”
“Unaitwa nani?”
“Humuli Samaki.”
“Unahamia peke yako au uko na mke na watoto?”
“Peke yangu mama.”
“Humuli Samaki ni mwanyeji wa wapi?”
“Usukumani.”
“Haya, naamini uliaga wakati unaondoka nyumbani.”
“Hilo lilikuwa la kwanza mama.”
“Haya, kila la kheri.”

Tuliendelea na kazi ya kuingiza vyombi ndani hadi tukamaliza. Wale wenye gari wakaondoka, nikabaki mimi peke yangu.

Nilijiwekea malengo kwamba, nihakikishe naweka sawa kila kitu ili kesho yake nisiwe na kazi hiyo zaidi ya kwenda kazini. Niliifanya kazi kwa muda wa saa tatu, mpaka kwenye saa saba na nusu usiku nikamaliza.

Nilibadili nguo, nikavaa taulo na kwenda kuoga. Nilikuta bafu limetoka kutumika kama dakika kumi nyuma, sikushangaa kwani si kuna wapangaji wengine ambao tulitakuwa kutumia bafu moja.

Usiku kabla ya kuzima taa, nilizima taa, nikapanda nitandani. Kabla sijapata usingizi, niliwasikia wenzangu wakicheka sana na kuongea huku wameweka muziki. Lakini ule muziki haukuwa wa kiarabu, kizungu wala kiswahili.

Hata maongezo yao, mimi nilisikia sauti tu lakini kusema walikuwa wanatumia lugha gani si rahisi. Kuna wakati kama walikuwa wakiongea kihindi, pia niliwasikia kama wanaongea kiarabu, nikajua ni watu wa namna hiyo.

Lakini sikulala mpaka nikampigia simu dalala kumuuliza kama wale wapangaji wenzangu ni weupe au waswahili kama mimi, akasema hata yeye hajui kwani hakuwahi kuwaona hata siku moja.

Basi, nililala. Asubuhi niliamka nikiwa nimechoka sana. Wakati nakwenda bafuni kuoga niligundua ni mimi peke yangu ndiye niliyekuwa nimetangulia kuamka, kwani bafuni hakukuwa na maji yaliyomwagika kwa muda huo.
Baada ya kuoga nilirudi chumbani kwangu kujiandaa kwenda kazini. Wakati najiandaa, nilisikia mlango ukifunguliwa, nikajua ni wenzangu wanakwenda kuoga au chooni kama ilivyo kawaida kwa wanadamu wakiamka asubuhi.

Niliamua kutumia nafasi hiyo kuwatambua. Nilivizia pale niliposikia mlio wa maji bafuni na mimi nikatoka kwenda kupiga mswaki kwa mara ya pili. Sehemu niliyosimama, mtu akitoka bafuni kwenda ndani ilikuwa lazima nimuone kwani ilikuwa kiasi cha kugeuka tu.

Lakini cha kushangaza, nilikuwa sisikii maji kumwagika, nikageuka na kuuna mlango wa bafuni upo wazi. Mbali na mlango kuwa wazi, pia chini nikaona alama za kandambili nne zikiwa zimekanyaga, nikajua wametoka.

“Lakini wamepitaje hapa?” nilijiuliza.
Nilirudi ndani, mlangoni kwao nilikuta kandambili pea mbili zikiwa bado na majimaji kwa mbali, jambo hili lilinifanya nijiuliuze sana.

Nilijipa ujasiri na kuamua kuchungulia ndani ya chumba hicho kwa kutumia nafasi ya katikati ya mlango ambapo niliweza kuona hadi kitanda lakini sikumwona mtu mwingine.
Niliingia kwangu, nikaweka mswaki, nikava vizuri na kuondoka zangu. Nilitegemea wenzangu nimewaacha ndani, kwani nilipofika mlangoni nilikuta umefunguliwa na upo wazi. Nilirudi ndani hadi kwenye mlango wao.
“Wa ndugu,” niliita kwa sauti.
“Jamani wa ndugu.”

Ukimya ndiyo ulinifanya nibaini walishaondoka. Kwani kulikuwa kimya sana na kandambili zilikuwa pembeni ya mlango si pale pa kwanza.

Nilifunga mlango mkubwa nikaondoka, mbele nilimwona yule mama aliyekuja usiku kuniuliza maswali. Alikuwa amesimama nje ya nyumba yake, aliponiona akashutuka na kuita majina mawili ya watu. Wakatoka watoto wake wawili, ni mabinti wenye miaka kama kumi na nane na ishirini na mbili hivi.

“Hujambo kijana?” yule mama alinisalimia kwa furaha.
“Sijambo mama, shikamoo.”
“Marhaba.” Kisha akawaambia kitu wale watoto wake nao wakanikazia macho.
“Mama umewaona majirani zangu hapa?”
“Majirani zako akina nani?”
“Wapangaji wenzangu.”
“Kijana, kua uyaone ya dunia. We si umeshakua, utayaona ya dunia.”
Kauli hiyo iliniogopesha sana, nikashtuka na kumuuliza mama.
“Mama una maana gani?”
“Sisi hatutaki umbeya kijana.”

“We si umeambiwa utayaona kwa hiyo subiri tu,” alidakia binti yake mkubwa.
Miguu ilitetemeka, mwili uliisha nguvu, nikajikuta nataka kukaa, lakini sikuweza. Nilichoamua ni kuondoka huku nampigia simu yule dalali.
“Vipi hujambo bwana?”
“Mimi sijambo.”
“Za makazi mapya.”
“Si nzuri bwana.”
“Kwanini tena?”   
“Sielewielewi.”
“Kivipi?”
“Kuna mambo kama si ya kawaida.”
“Yapi hayo?”
“Wale wapangaji wenzangu siwaelewi kabisa.”
“Kivipi?”
“Ah! Watu gani mimi mgeni nimehamia washindwe kutoka kunisalimia ili angalau tufahamiane?”

Dalali alicheka sana kisha akasema:
“Wale ndivyo walivyo bwana, si unajua tena malezi, mwingine kalelewa vile, mwingine hivi. Ila ulichokisema ni kweli, haiwezekani nyumba mnayoishi mpate mgeni halafu msitambuane, sasa mkikutana njiani je?”

“Si ndiyo hapo sasa,” nilisema nikijifanya lawama zangu ni kwa ajili ya hilo tu, lakini kumbe nilikuwa na zaidi ya hapo.

Kazini siku hiyo nilishinda sina amani, sina raha, mwili ulikuwa kama umetoka kufanya kazi nzito ambayo sijawahi kuifanya kwa siku nyingi, wenyeji wa Pwani wanaita mavune.
Kwa upande mwingine nilitamani sana jioni ifike ili nikaone siku hiyo kitatokea kitu gani kipya kwenye nyumba ile. Jioni ilifika, nikaondoka kazini, sikutaka kupitia popote, dukuduku langu lilikuwa kwenda nyumbani tu.

Nilichukua kama saa moja kutoka kazini hadi kufika nyumbani. Nje nilikuta mfuko wa rambo  mweusi, ndani yake ulionekana kuwa na kitu kwani ulikuwa umetuna sana. Niliinama kuipekenyua ili nijue ndani kulikuwa na nini, nilishangaa kuona ni vipande vya nyama za kuchoma tena vilikuwa na moto.
“Kha! Atakuwa nani ameweka?”
 Usikose sehemu O2 

Urusi: Shambulio la ndege ya Syria ni uchokozi

Urusi imeitaka Marekani kuheshimu uhuru na mipaka ya Syria baada ya kuangusha ndege ya jeshi la Syria katika mkoa wa Raqqa. Ndege hiyo  ilikuwa katika harakati za kushambulia kundi linalojjita dola kiislamu IS.

Russland Treffen von Lavrov, Javad Zarif und Muallem in Moskau (Reuters/S. Karpukhin)

Akizungumza katika mkutano wa mawaziri wa maswala  ya kigeni mjini Beijing nchini China,waziri wa mambo ya kigeni wa Urusi Sergei Lavrov amesema shambulizi hilo na Marekani dhidi ya ndege ya jeshi la Syria  huenda likazidisha mzozo nchini Syria na pia kuhatarisha vita dhidi ya ugaidi. Kisa hicho  kimetokea  wakati ambapo majeshi ya Syria yameimarisha mashambulizi yake dhidi ya wapiganaji wa IS kusini na magharibi mwa  Raqqa, huku nalo jeshi la waasi wa Syria lijulikanlo kama Syria Democratic forces linaloungwa mkono na Marekani likiendeleza  vita  dhidi ya kundi kundi hilo  la IS ndani ya mji wa Raqqa,ambao ndio ngome ya wapiganaji hao wa IS. Katika taarifa Marekani imesema ilichukua hatua za kujilinda baada ya majeshi hayo ya Syria kuangusha mabomu karibu na  eneo linalosimamiwa na jeshi la waasi la Syria Democratic forces.

Syrien Demokratische Kräfte Syriens bei Raqqa (picture-alliance/AP Photo/Syrian Democratic Forces)

Waasi wa jeshi la Syrian Democratic Forces wakipiga doria mji wa Raqqa

Marekani pia iliweka wazi kuwa haiyalengi majeshi ya Syria au Urusi, na iwapo  muungano wa vikosi vyake utahitajika kufanya mashambulizi ya kujilinda basi havitasita kuchukua hatua.

Marekani inaunga mkono magaidi

Hata hivyo kamanda wa jeshi la Syria amelitaja shambulizi hilo dhidi ya ndege ya Syria kama ushahidi wa jukumu la Marekani katika kuunga mkono wapiganaji wa IS.Jeshi la Syria  limeonya kutokea madhara makubwa kufuatia shambulizi hilo, na kusisitiza  kuwa vitendo kama hivyo  havitalizuia kuendelea na  harakati zake za kupiga vita makundi ya kigaidi na kurejesha amani na usalama  kwa wa Syria wote.Saa chache kabla ya kuangushwa kwa ndege hiyo ya jeshi ya Syria,

Syrien Flüchtlinge aus Rakka bei Ain Issa (Reuters/R. Said)

Wasyria wanaokimbia vita mji wa Raqqa

Marekani ilisema kuwa vikosi vinavyomuunga mkono rais wa Syria Bashar al-Assad viliwashambulia wanajeshi wa jeshi la  waasi la Syria Democratic forces  na baadhi yao kujeruhiwa. Mapema mwezi huu, Marekani iliangusha ndege isiyo na rubani ya serikali ya Syria, baada ya ndege hiyo kushambulia vikosi karibu na kivuko cha mpaka cha al-Tanf kwenye mpaka kati ya Syria na Iraq.Taarifa nyingine ni kuwa jeshi la Ukombozi  la Iran limetoa onyo kali dhidi ya wapiganaji wa IS,na kusema mashambulizi yeyote dhidi ya Iran yatailazimisha kutumia nguvu zaidi.Tangazo hilo lilitolewa baada ya jeshi hilo la Iran  kurusha makombora yaliyolenga kundi hilo la IS mashariki mwa Syria. 

Chanzo. Dw.de

HADITHI; Niliolewa na Jini bila ya kutarajia - 12


NILIOLEWA NA JINI BILA YA KUTARAJIA 12

Mara gafla nikaona mlango wa chumba changu ukifunguliwa, muda huo huo mkojo ulinitoka bila ya hodi.
Nilikuwa nangoja kuona huyo mtu wa ajabu atakayeingia ndani kwani nilijua kuwa kwa vyovyote vile siwezi kumkwepa.


Mlango wangu ulikuwa unafunguliwa polepole, ujasiri ukaniisha na kujifunika sura kwani sikuweza tena kutazama kitu kitakachoingia, mara nikashikwa kichwani na hapo nikapiga ukelele uliomuamsha hadi mama.


Mama akafika chumbani kwangu wakati mimi nikiwa bado nimeinama na kujikunyata.
"Vipi mwanangu jamani? Umepatwa na nini tena? Eti Penina, mdogo wako amepatwa na nini?"
Mama alimuuliza dada Penina ambaye naye alikuwa chumbani kwangu.


"Hata mimi namshangaa jamani, mi nilikuja chumbani kwake huku na nikafungua mlango taratibu ili nisimsumbue, shida yangu ilikuwa ni ile pochi ndogo. Nimeshangaa kumkuta hapo chini amejikunyata na kujiinamia nikaamua kumshika kichwani ili kumuangalia ana tatizo gani ila ile kumshika tu ndio akapiga makelele yote hayo.


Mama akaniangalia kwa makini,
"Kwani una nini Sabrina? Au kuna mambo ulikuwa unayawaza?"
Kitu cha kwanza kuwauliza ilikuwa ni muda,
"Kwani saa ngapi saizi?"
"Kumekucha mwanangu na dada yako ndio huyu amejiandaa kwenda kazini"
Nikabaki nashangaa tu na sikuelewa chochote, mama akaangalia chini na kuona yale majimaji ya mkoje.


"Kheee! Hadi umejikojolea Sabrina!! Ulikuwa unaogopa nini mwanangu?"
"Amejikojolea kweli loh"
Dada akaanza kucheka, kisha akachukua alichosema na kuondoka.
Nikabaki na mama tu pale ndani.


Kulipokucha vizuri nilikuwa nimeshaoga na kutafakari ya usiku kwakweli hakuna ambacho nilikuwa nakielewa. Nikaenda kwa mama jikoni kumuuliza,
"Nitaenda lini kwa kaka Deo mama?


"Sabrina mwanangu, umeanza uoga hadi wa kufikia kujikojolea si utaenda kutia aibu tu huko kwa kaka yako? Sidhani kama wifi yako atavumilia hali hiyo!"
"Mama yani bahati mbaya ya siku moja ndio unaihesabia kama siku zote? Mimi nataka kwenda kwa kaka haijalishi nini wala nini"
"Utaenda ila ndio hivyo utatutia aibu kama ukiendeleza hiyo tabia"
Nikamsikiliza mama ila moyoni bado nilitaka kwenda kwa kaka tu ili nibahatike kubadilisha mazingira kidogo.


Mchana nikajilaza sebleni kwani macho yangu yalikuwa mazito sana na kujawa na usingizi.
Mama akanishtua kuwa nimepata ugeni, kuamka nikamkuta ni Carlos ambapo mama alimkaribisha sebleni tayari.


Kisha mama akaenda chumbani kuendelea na mambo yake mengine, Carlos akaanza kujiongelesha pale.
"Mbona umechukia Sabrina? Hujaupenda ujio wangu?"
"Hapana, ila mbona umekuja bila taarifa?"
"Nimekuja kuangalia unaendeleaje Sabrina, nakujali sana mama angu. Nikwambie kitu Sabr."
"Niambie tu hakuna tatizo"
"Sabrina, wewe kweli ni binti mzuri na mrembo yani ingawa umetoka kulala ila bado unapendeza na kuvutia. Sura yako ina mvuto wa hali ya juu Sabrina, na umbo lako ni zuri sana ila samahani kama sifa zangu zimevuka mipaka.


Nikacheka na kumuangalia vizuri huyu Carlos ambaye leo alikuja na staili ya kunisifia.
Nikaamua kumuuliza swali Carlos,
"Mbona umeamua kunisifu kiasi hicho?"
"Anayestahili sifa acha apewe sifa yangu, kwakweli Sabrina hadi nimekupenda yani."
Nikashtuka na kumuuliza tena.


"Si unajua kama mimi nipo na Sam halafu tunapendana sana?"
"Tatizo lenu wasichana ndio hilo, mtu akitamka nakupenda basi wewe ushapelekea kwenye maana nyingine. Mimi nakupenda Sabrina kama Sabrina na si vinginevyo.


Nikabaki kimya kwani alinishushua, akaongea mambo mengine kisha akaondoka.
Nikawa naitafakari ile kauli ya Carlos ya kusema kuwa ananipenda Sabrina kama Sabrina na si vinginevyo, kauli yake bado ilikuwa na utata sana kichwani mwangu ila sikupenda kuijadili zaidi.

Jioni yake Carlos akanipigia simu na kuniuliza.


"Unapenda chocolate Sabrina?"
"Ndio nazipenda."
"Nikuletee?"
Nikasita kuitikia nikawa kimya tu na simu sikioni,
"Basi nakuletea"
Halafu akakata simu, nikawa nashangaa tu kwani bado sikuwa na imani nzuri na Carlos.
Haikuchukua muda nikamsikia Carlos akizungumza na mama.


"Mimi sio mkaaji mama, nimemletea Sabrina mzigo wake huu."
Kisha nikamsikia akiaga, baada ya muda kidogo mama akaniita huku akiufungua ule mzigo.
"Mmh kumbe chocolate, huyu ndio mkwe bwana sio huyo Sam wako."
Akafungua moja wapo na kuanza kula huku akinikabidhi ule mfuko, ila mimi nikakataa na kumuachia mama.


Dada yangu Penina nae aliporudi wakaungana na mama kula zile chokleti. Na mimi nikatumia mwanya huo kumchombeza mama,
"Leo mama tutalala wote eeh!!"
"Hakuna shida mwanangu tutalala tu, ila masharti yale yale kuongea na simu usiku sitaki."
"Sawa mama hakuna tatizo"
Nikatulia pale sebleni na kuwaangalia tu walivyokuwa wakisakamia zile chokleti huku wakisifu kuwa ni tamu sana.


Usiku ulipowadia, nilijipanga kulala na mama ila nilimkumbuka sana Sam nikaamua kumpigia simu kabla ya kulala ila haikupatikana.
Mawasiliano yangu na Sam yamekuwa yakisuasua sana kwa siku mbili tatu hizi hata nikishindwa kuelewa kuwa Sam atakuwa amepatwa na tatizo gani jingine.


Nikaenda kulala chumbani kwa mama ambaye alinisihi kuwa nisiwe muoga, kitu cha ajabu kwetu ilikuwa tunakumbuka vyote ila si kusali tena mara nyingine kukishakucha mama ndio anakumbuka kuwa hakufanya ibada.


Niliongea na mama pale mambo mawili matatu na kisha kulala.

Kama kawaida yule mkaka wa ndotoni alinitokea na kunifata mahali ambapo nilikuwa nimekaa katikati ya nyasi laini na nyororo, yule mkaka akaanza kusema.
"Nikupe kitu gani Sabrina ili ujue kama nakupenda? Nikuonyeshe ishara gani ili utambue upendo wangu kwako?


Nikawa namuangalia tu bila ya kumjibu chochote kile.
"Ninauwezo mkubwa sana wa kukufanya mke wangu hata kama hutaka ila mimi nahitaji ukubali kwa hiyari yako mwenyewe"
Akaanza kuongea maneno ambayo yalifanana na aliyoongea Carlos mchana.
"Sabrina, wewe ni binti mzuri na mrembo. Una sura ya kuvutia na umbo."
Kisha akamalizia kuwa.


"Anayestahili sifa apewe sifa yake"
Nikashtuka kutoka usingizini na kuhema juu juu.
Nikaanza kumfikiria Carlos, sura yake ikatembea mawazoni mwangu na ule ubaridi wa mikono yake nikaanza kuuhisi mwilini mwangu hadi kuanza kutetemeka.


Nikajiuliza maswali mengi sana juu ya Carlos, mara nikaona kivuli cha mtu mule chumbani kwa mama hapo sasa uoga ukanishika na kuanza kutetemeka, kile kivuli kikawa kinanisogelea taratibu yani kinakuwa kirefu nikawa nimemkumbatia mama na mara ikasogea hdi usoni kwangu na kunichekea.


Hapo sasa nikaanza kumuamsha mama kinguu ila mama alikuwa hoi kabisa hata hajitambui na hakuamka kabisa ikawa kama vile niko peke yangu mule chumbani.
Ikaanza sauti ya paka kama ile ambayo uwa inasikika chumbani kwangu, hapo nikazidi kutetemeka na kuzidi kumkumbatia mama.


Kwakweli leo nilimshangaa mama kwani hakushtuka hata kidogo tofauti na siku zingine, na gafla umeme ukakatika hapo ndipo uoga ulipozidi na kuendelea kumuamsha mama ambaye aliamka na kuongea kama mlevi kisha kulala tena.


Katika hali ile ya uoga nikapitiwa na usingizi palepale.

Yule mkaka wa ndotoni alikuwa anacheka sasa tena akicheka sana sana, kisha akaniambia nimpe mkono wangu nikasita kumpa na kukataa kabisa, akaniambia.
"Nakupenda Sabrina"
Nikamuangalia tu, akawa analazimisha kuwa nimwambie nampenda nikagoma akawa anataka kunichukua kwa nguvu.


Nikashtuka na kupiga kelele,
"Nampenda Sam"
Hapo mama nae akashtuka na kuniangalia kwa jicho kali sana.
"Yani wewe asubuhi Sam, mchana, jioni khee hadi ndotoni? Huyo Sam kakupa nini mwanangu?"
Akiuliza hayo, alikuwa akiangalia mwanga uliokuwemo chumbani na kugundua kuwa kumeshakucha teyari, akastaajabu sana kuona amepitiliza kulala kiasi kile.


Nikaenda kumuangalia na dada Penina ambaye nae alikuwa hoi na usingizi, nikamuamsha naye alishangaa kuona kumekucha kuasi kile.
"Mmh nimelala kama mlevi leo jamani"
Nadhani na wao hawakujielewa kama mimi niotaye ndoto za ajabu tu.


Siku ya leo kila mtu alikuwa na mawazo nyumbani kwetu, sijui na wao walipatwa na mandoto ya ajabu kama yangu. Nikawa nimetulia na kutafakari, ikaingia simu kuangalia mpigaji ni Lucy. Ile kupokea tu akanipachika swali,
"Sam unampenda humpendi?"
"Swali gani hilo la kuniuliza Lucy?"
"Kila swali ni swali na linahitaji majibu, jibu swali nililokuuliza.


"Unajua wazi jinsi gani nampenda Sam"
"Kama unampenda mbona unamsababishia majanga?"
"Majanga? Majanga gani?"
Lucy akakata simu, nikajaribu kumpigia Sam hakupatikana.


Nikampigia tena Lucy naye hakupatikana na kujikuta nikiwaza vitu vingi mno.

Nikafikiria sana na kukosa jibu, nikaamua kuvaa ili niende kwa Sam.
Kwavile ilikuwa ni jioni sana yani karibia na usiku, mama akanikatalia kutoka. Nikajikuta nikiwa na mawazo sana na roho kuniuma, muda wote nilimjaribisha hewani Sam alikuwa hapatikani wala Lucy nae hapatikani.


Siku hiyo nilikaa na dada kwenye luninga huku nikiwa na mawazo tu, ila badae dada alienda kulala na kuniacha mwenyewe pale sebleni. Saa sita usiku nikaamua kumtafuta tena Sam hewani na muda huu simu yake ikaita nikafurahi sana ili niweze kuongea naye na kupunguza mawazo yangu ila cha kushangaza hakupokea Sam bali ilipokelewa na Lucy.


"Sema shida yako haraka tunataka kupumzika bhana."
Niliiweka ile simu sikioni huku nikiwaza kuwa huyu ni Lucy kweli au yule jamaa wa kujigeuza. Mara nikashikwa bega na ile mikono ya baridi.

Itaendelea kesho......!!!!
Kama tuko pamoja   
By, Atuganile Mwakalile.

HADITHI; Niliolewa na Jini bila ya kutarajia - 11


NILIOLEWA NA JINI BILA YA KUTARAJIA 11:

Nilipogeuka ili kuondoka tu akanishika mkono na mkono wake ulikuwa wa baridi sana.
Ubaridi ule ulipenya kwenye mwili wangu hata nilihisi baridi na mimi, Carlos akaniangalia kwa makini kana kwamba anayasoma mawazo yangu.


"Mbona unaniogopa Sabrina? Mimi ni binadamu wa kawaida kama wengine jamani."
Nilibaki nikimuangalia tu, bila ya kumjibu kitu chochote.
"Kwani mimi nina pembe jamani? Au natisha? Kwanini uniogope Sabrina?"
Nikazidi kumuangalia na kuanza kumuuliza maswali na mimi.


"Kwani wewe ulijuaje kama simu yangu ilianguka?"
"Kwahiyo hicho ndio kinafanya uniogope?"
"Na je namba yangu uliitoa wapi?"
"Sikia Sabrina, siku niliyochukua simu ya Sam kuweka namba yangu ndio nikachukua namba yako humo. Halafu siku ile niliyokupigia nilijua tu umeshtushwa na simu yangu kwani nikasikia kama simu imeanguka na gafla ukapotea hewani ndipo nilipogundua kuwa simu yako imeanguka na kuharibika.


 Roho ikaniuma sana kwani mimi ndiye niliyesababisha ndiomana nikaamua kwenda kukununulia simu nyingine kama ishara ya kuomba samahani. Tafadhari Sabrina pokea simu hii"
Ingawa nimeyaelewa maelezo ambayo Carlos ameyatoa ila bado iliniwia vigumu kupokea ile simu.
Mara mama akatoka ndani na kunikuta nimesimama na Carlos pale nje.
"Yani Sabrina muda wote umesimama na mgeni hapo nje? Kwanini usiingie nae ndani mwanangu! Haya karibu ndani baba.


Nikajua mama ameshapagawa na lile gari la Carlos pale nje, ikabidi nimkaribishe Carlos ndani ingawa sikuwa na imani nae.

Tukiwa tumekaa pale sebleni, mama akaanza kumuuliza maswali mawili matatu Carlos.
"Kwani wewe ni mwenyeji wa wapi baba?"
"Mimi ni mwenyeji wa mkoa wa Kigoma"
"Wazazi wako wako wapi?"
"Wazazi wapo Kigoma ila nina ndugu zangu baadhi hapa na wazazi nao watakuja tu maana wamekaa sana kule na wameshapachoka"
Carlos aliongea mambo mengi sana na mama, hadi kumwambia kuhusu simu aliyoniletea.
Mama nae akaanza kunilazimisha kuwa nichukue simu ile niliyoletewa na Carlos.
"Yani mama, mi sina nia mbaya kabisa kumletea Sabrina simu. Nimefanya hivi kama ishara ya urafiki wetu tu.


"Ndio namshangaa hapa kinachomfanya akatae, labda anahisi utamdai."
"Siwezi kumdai mama, nimemletea hii simu kwa hiyari yangu mwenyewe"
Mama akaendelea kunisisitiza kuwa niichukue, ikabidi niichukue ile simu na kumuuliza swali ambalo lilinitatiza bado.


"Mbona mikono yako ni ya baridi sana?"
"Hutokea tu ila si mara zote, nadhani nina upungufu wa madini flani mwilini"
Mama akaanza kucheka kisha Carlos akaaga na kuondoka.

Nilitafakari vitu vingi sana bila ya kupata jibu, kwakweli huyu Carlos alinifikirisha sana tena sana, hata nikashangaa kuwa mama amewezaje kumuamini Carlos kwa muda mfupi kiasi kile.
Mama akaja na kuanza kuniambia.


"Maskini jeuri wewe, simu unaitaka halafu unavunga! Kaka wa watu kajitokea mbali kwaajili yako eti wewe unavunga loh"
"Ila mimi simuamini yule kaka kabisa"
"Kwanini humuamini? Mbona ni mtu wa kawaida tu mwanangu!"
"Mi simuamini tu jamani"
Kwakweli sikumuamini kabisa Carlos niliona ni majanga tu.


Usiku ulipofika, mama alikuja kutembelewa na rafiki yake mama Salome.
Mama akaanza kumuelezea kuhusiana na matatizo yangu ya kuogopa ndani.
Nilikuwa kimya kwenye kochi nikijifanya nimesinzia ila nilisikia yote waliyozungumza.
"Sasa mama Penina, kama mtoto anawehuka hivyo wakati wa kulala kwanini msifanye maombi?"
"Hapo ndio hadi mi mwenyewe najishangaa mama Salome, yani Sabrina akianza kuwehuka huwa sikumbuki kabisa kusali hata sijui kwanini?


"Dunia imechafuka sana ndugu yangu, shetani ana jeshi lake kubwa humu duniani inatakiwa mkumbuke kusali kwani sala ni nguzo imara ya kumpinga shetani."
"Asante mama Salome nitafanyia kazi ulichosema"
"Tena kwa ushauri wa bure, ita familia yako tulia nayo mnaomba pamoja halafu mnalala"
"Nimekuelewa ndugu yangu.


Mama Salome akaaga na kuondoka kwani alikuja kumwambia mama habari za kikundi chao ila mazungumzo haya mengine yaliingilia kati tu.

Dada akarudi nyumbani, kwakweli leo alichelewa sana kurudi na alitukuta tunakula ilibidi mama amuulize sababu ya kuchelewa.
"Kuna mambo ya Fatuma namsaidia kushughulikia, nadhani kesho au keshokutwa tunaweza kufanikisha"
"Mambo gani hayo?"
"Nikiyasema sasa hivi kuna shoga yangu hapa atasema namtisha asilale, nitawaambia kesho kama nikirudi mchana"
Nikajua tu hayo mambo lazima yatakuwa yanahusiana na majini tu ndiomana hajayaongelea kwani anajua kuwa mimi naogopa sana mambo hayo.


Muda wa kulala ukafika, mama akainuka kwenda kulala na kuniacha na dada pale sebleni. Nikakumbuka maneno ya mama Salome kuwa tupende kusali kabla ya kulala, nikamfata mama na kumwambia kuwa amesahau maagizo aliyosema kwa mama Salome kuwa atayatelekeza.
Nikamkumbusha mama kusali naye akakumbuka, akarudi sebleni na kumwambia dada Penina kuwa tunatakiwa kusali kabla ya kulala.


"Mama, kila mtu atabeba mzigo wake mwenyewe, maswala ya kulazimishana kusali mimi hata siyapendi"
Dada Penina akawa anapinga kabisa ikabidi mama amuombe na kumlazimisha kuwa ni vyema tukifanya ibada ya pamoja, badae akakubali.


Kama familia tukaamua kufanya ibada kabla ya kulala.

Wakati wa ibada hiyo hakuna aliyeelewa nini kiliendelea kwani kila mmoja alijikuta yupo chumbani kwake asubuhi, na mama ndiye aliyekuwa wa kwanza kuja chumbani kwangu.
"Hivi muda ule tuliosema tunafanya ibada ilikuwaje?"
"Hata sielewi mama, maana sina kumbukumbu za ibada hiyo."
"Mmh ya leo kali!"
Dada Penina nae aliamka na kuja chumbani kwangu.


"Leo nimechelewa hadi kwenda kazini sijui hata ni usingizi wa aina gani!"
"Kila mmoja anashangaa hapa maana mara ya mwisho tulipanga kufanya ibada"
"Au tulifanya ibada na kwenda kulala?"
"Labda ila hakuna mwenye kumbukumbu yoyote."
Mimi nilikuwa natafakari tu na nikatambua kuwa yote yanafanywa na yule mkaka wa ndotoni tu kwani tuo afanyaye mambo ya ajabu.


Mchana nikampigia simu Sam, ambaye alikuwa na mawazo ya kupotelewa na pesa ya ofisi.
"Yani nimechanganyikiwa Sabrina, hata sijui pesa ya ofini nitaipatia wapi tena jamani mmh!"
Nikajaribu kumpa moyo na kumwambia maneno mazuri ambayo najua hayakumfariji hata kidogo kwani alikuwa ameshachanganyikiwa.


Nikapigiwa simu na rafiki yangu Suzy ambaye alianza tena kuniuliza kuhusu Carlos.
"Sabrina, unamuonaje Carlos?"
"Namuona ni mtu wa kawaida tu, kwani wewe unamuonaje?"
"Ngoja kwanza, nikimaliza uchunguzi wangu nitakwambia"
Suzy akakata simu, nikajiuliza maswali kuwa kwanini Suzy ana wasiwasi juu ya Carlos.
Mama akaniita na kuniambia kuwa ameongea na kaka na amesema kwamba hivi karibuni atanihitaji kwake ili nikabadilishe mazingira kidogo, kwakweli nilifurahi sana, hata dada aliporudi aliona jinsi nilivyofurahi.


Wakati wa kula dada akaamua kunitani,
"Naona umefurahi kuepukana na stori zangu za kutisha."
Mama akadakia,
"Lazima afurahi, anavyoogopa majini na watu waliofufuka huyu balaa"
Yani wanavyosema watu waliofufuka mie mwenzao ndio nazidi kupatwa na uoga wa mawazo.
"Anaogomba mazombie mdogo wangu jamani, ila mama yanatisha kweli yale usiombe ukutane nao


"Majini yako je hayatishi?"
"Mama wee usiniambie habari za majini, kilichompata Fatuma ni balaa"
"Mmeshaanza stori zenu sasa, mi mnanikera sana"
Ikabidi wanyamaze na tuendelee kula kama kawaida.

Usiku mawazo yangu yalikuwa ni kwenda kwa kaka tu, sikuwa na mawazo mengine zaidi ya hayo na sikutaka kukaribisha mawazo ya zaidi.
Wakati wa kulala ulipofika, nilikwenda chumbani na kulala moja kwa moja hata simu sikuongea nayo usiku.


Nikamuona Sam akihangaika sana, mara nikamuona akifunga ndoa na Lucy halafu tena nikamuona akitokwa na majipu mwili mzima. Nikashtuka kutoka kwenye ile ndoto na kujikuta nikianza kuogopa mule nyumbani, kwani wakati nimeshtuka nilikuwa nahisi kama mtu akitembea tembea mara avute kiti mara avute meza halafu sauti ikasika.


"Mbona umeamka kabla ya wakati Sabrina?"
Uoga ukanijaa, nikakumbuka maneno ya mama Salome kuwa natakiwa kusali.
Nikashuka kitandani na kupiga magoti, kabla sijafanya chochote taa ya chumbani ikazimwa halafu mikono ya baridi ikawa inagusa miguu yangu.


Kwakweli nilitetemeka kiasi cha kupoteza fahamu, sikupenda kutazama mbele na mara taa zikawashwa tena hapo nilizidi kutetemeka na hakuna maombi tena niliyoweza kuyafanya.
Nilijikunyata ukutani bila ya kujua cha kufanya, ile sauti ikajirudia tena.
"Mbona umeamka mapema Sabrina"
Kwakweli huu usiku ningeweza kuubadilisha basi ningeubadilisha jamani, jasho jingi lilinitoka na wakati nilikuwa natetemeka kwa baridi la uoga.


"Usiogope Sabrina, nipo nje ya chumba chako bado sijaingia ndani ila karibia nitaingia"
Mara gafla nikaona mlango wa chumba changu ukifunguliwa, muda huohuo mkojo ulinitoka bila ya hodi.

Itaendelea kesho......!!!
Kama tuko pamoja   
By, Atuganile Mwakalile.


 
 
Blogger Templates