Social Icons

Tuesday 30 January 2018

Kiapo cha Odinga ni 'kinyume cha sheria'- Serikali


Serikali ya Kenya imeviamuru vyombo vya habari kutopeperusha mubashara kuapishwa kwa kiongozi wa upinzani (Nasa) kama “Rais wa Wananchi” ambako kumepangwa kufanyika Januari 30, 2018, chombo cha habari cha binafsi NTV kimeripoti.

“Rais Uhuru Kenyatta na makamu wake William Ruto wamefanya mkutano wa pamoja na Waziri wa Usalama wa Ndani Fred Matiang’i, Waziri wa Habari na Mawasiliano ya Kiteknolojia Joe Mucheru na Mwanasheria Mkuu Githu Muigai kwa lengo la kuvitaka vyombo vya habari kujizuilia kutangaza kuapishwa kwa Raila Odinga na Kalonzo Musyoka kuliko andaliwa na Nasa,” NTV imeripoti.

Televisheni imesema kuwa mkutano huo ulikuwa umefanyika katika ikulu ya rais Januari 26, muda kidogo kabla ya Kenyatta kutaja majina ya baraza lake la mawaziri.

“Mkutano huo pia ulihudhuriwa na wakurugenzi; Rose Kimotho wa Kampuni ya habari Three Stones Media, Cyrus Maina wa Kituo cha radio cha Capital FM, Ian Fernandez wa Kituo cha habari K24 na mkurugenzi wa Kampuni ya Nation Media Group Tom Mshindi,” ripoti hiyo imeeleza zaidi.

NTV imesema kuwa serikali imeonya kuwa wale watakao tangaza sherehe hizo za kuapishwa ambazo ni “kinyume cha sheria” huko katika eneo la Uhuru Park vituo vyao vitafungiwa.

Nasa imeahidi kukaidi amri ya serikali inayopiga marufuku kuapishwa huko.

Upinzani umesema utaendelea na sherehe hizo za kuapishwa huko eneo la Uhuru Park katika mji mkuu wa Nairobi, pamoja na mamlaka husika kusema kuwa eneo hilo limefungwa kwa ajili ya kufanyiwa ukarabati kwa kipindi hadi katikati ya mwezi wa Februari.


Chanzo. VOA

No comments:

 
 
Blogger Templates